HEADLINES

6/recent/ticker-posts

SERIKALI KUENDELEA KUTENGA FEDHA ZA UBORESHAJI WA HIFADHI ZA TAIFA CHANGA

 Na Mwandishi Wetu,

DODOMA,


Serikali kupitia fedha za Mpango wa Maendeleo na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 inaendelea na mchakato wa kuboresha hifadhi changa 17 za Taifa ikiwemo kuboresha miundombinu ya barabara, huduma za malazi na chakula na maeneo ya uwekezaji kwa lengo la kukuza utalii na kuongeza mapato. 

Hayo yamesemwa leo Aprili 4, 2023 Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Jacqueline Andrew aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kutenga bajeti kwa ajili ya kuboresha Hifadhi za Taifa changa  ili kukuza utalii.

Amezitaja Hifadhi za Taifa zinazoboreshwa kuwa ni Burigi-Chato, Gombe, Ibanda-Kyerwa, Katavi, Kigosi, Kisiwa cha Rubondo, Kisiwa cha Saanane, Kitulo, Milima ya Mahale, Milima ya Udzungwa, Mikumi, Mkomazi, Mto Ugalla, Nyerere, Ruaha, Rumanyika-Karagwe na Saadani. 

Aidha, amefafanua kuwa maboresho yanayofanywa katika hifadhi hizo yanaenda sambamba na utekelezaji wa Programu ya Tanzania – the Royal Tour ambapo kwa sasa Serikali imejikita zaidi kwenye maeneo mapya ya utalii.


Post a Comment

0 Comments