HEADLINES

6/recent/ticker-posts

BASHUNGWA: MAMENEJA WA TANROADS WASIOSIMAMIA MIRADI KIKAMILIFU KUANZA KUCHUKULIWA HATUA


Na Mwandishi Wetu,
MOROGORO,

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amemuagiza  Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara (TANROADS), kuwachukulia hatua Mameneja wa Mikoa wanaoshindwa kusimamia usanifu wa kina na ujenzi wa barabara na madaraja kwa viwango na kupelekea miumbombinu kuharibika ndani ya muda mfupi.

Bashungwa ametoa maagizo hayo  Februari 22, 2024 wakati akikagua miundombinu ya barabara na Daraja la Nguyami ambalo mawasiliano yake yamekatika kutokana na mvua za El-nino zinazoendelea kunyesha, Wilayani Gairo, Mkoani Morogoro.

“Mameneja wote wa mikoa mhakikishe mnasimamia na kusanifu makalvati na madaraja ambayo yanastahimili na yanadumu kwa muda mrefu na Meneja yeyote ambaye atakuwa hasimamii miradi ipasavyo hata nikikuta umehamishwa mkoa nitakufuata huko huko kuja kukutumbua”, amesisitiza Bashungwa.

 Aidha, Bashungwa amemtaka Meneja wa TANROADS Mkoa wa Morogoro kuhakikisha hatua za manunuzi za kumpata Mkandarasi wa kujenga madaraja ya Nguyami  na Chakwale zinafanyika haraka ili kabla ya kuisha kwa mwaka wa fedha 2023/24 mkandarasi awe amekabidhiwa kazi na kuanza ujenzi mara moja.



Waziri Bashungwa amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatoa fedha ili kujengwa kwa madaraja ya kisasa ambaya yataunganisha Mkoa wa Morogoro na Tanga kupitia Gairo-Chakwale hadi Nguyami. 

Akitoa taarifa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Alinanuswe Kyamba, amesema upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa madaraja ya Chakwale na Nguyami ulikamilika mwaka 2022 na katika mwaka wa fedha wa 2023/24 Serikali imetenga fedha za kuanza ujenzi wa madaraja hayo.

Naye Mbunge wa Gairo, Ahmad Shabiby, amesema kukamilika kwa madaraja hayo kutafungua fursa za kiuchumi kwa wananchi katika Mkoa wa Morogoro kupitia Gairo na Kilindi Mkoani Tanga.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima amesema Mkoa umejipanga kusimamia miradi mbalimbali hasa ya barabara na madaraja yanayotekelezwa na TANROADS.



Post a Comment

0 Comments