HEADLINES

6/recent/ticker-posts


 Na Mwandishi Wetu,

DAR ES SALAAM.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila ameagiza mchakato wa kuwapata wafanyabiashara kuanza upya na ufanyike kwa uwazi na majina yatahuishwa kwa pamoja kwenye mfumo baada ya kupitiwa na Taasisi kadhaa kujiridhisha

-Aagiza TAKUKURU Mkoa kufuatilia kwa karibu Shirika la masoko Kariakoo

-Atoa wiki mbili Bodi na Mtendaji Mkuu wa Shirika la masoko Kariakoo kujitathimini

-Amtaka Katibu Tawala wa Mkoa Dkt Toba Nguvila kupitia taarifa za watumishi wa shirikia hilo kujua wamekaa kituo hicho kwa muda gani.

-Aagiza wafanyabiashara waliotumia ujanja kujipatia kibanda zaidi ya kimoja wachukuliwe hatua. 

Chalamila leo Julai 12, 2024 kwa nyakati tofauti amekutana na kufanya kikao na wafanyabiashara wadogo maarufu kwa jina la machinga na watumishi wa Shirika la Masoko ya Kariakoo.

 RC chalamila akiongea na wafanyabishara katika ukumbi wa ofisi yake Ilala Boma alipata wasaa wa kuwasikiliza kwa kina malalamiko na kuwahakikishia Serikali ya Mkoa iko makini sana mfanyabiashara ambaye atakuwa na janja janja ya kujipatia kibanda zaidi ya kimoja hatua kali zitachukuliwa dhidi yake “Kamwe siasa kariakoo hazikubaliki nitasimama imara” Alisema Chalamila.

Aidha RC Chalamila baada ya kuongea na mamia ya wafanyabiasha hao alifanya kikao kingine na watumishi wa shirika la Masoko Kariakoo ambapo ameagiza kushushwa kwa majina 891 kwenye mfumo ili kufanyika upya kwa uhakiki tena kwa uwazi ili kusiwe na malalamiko ya wafanyabiashara.

Sanjari na hilo RC Chalamila ameagiza TAKUKURU Mkoa kufuatilia kwa karibu Shirika la Masoko Kariakoo na kuitaka Bodi ya Shirika hilo pamoja na mtendaji mkuu ndani ya wiki mbili kuanzia leo kujitathimini juu ya malalamiko ya vitendo vya Rushwa yanayotolewa na wafanyabiashara kwa Shirika hilo.

Vilevile amemtaka Katibu Tawala wa Mkoa Dkt Toba Nguvila ndani ya wiki moja kupitia taarifa za watumishi wa shirika la masoko Kariakoo kujua wamekaa katika kituo hicho muda gani pia ufanisi katika utendaji wao wa kazi aidha ameelekeza wakati wa uhakiki mfanyabiashara atakayebainika kujipatia kwa ujanja kibanda zaidi ya kimoja achukuliwe hatua stahiki

Mwisho RC Chalamila amesema katika Soko la Kariakoo Serikali imefanya uwekezaji mkubwa kukarabati na kujenga Soko jipya hivyo uendeshaji wake lazima uwe wa kidigitali pia kila mmoja atambue soko la Kariakoo ni la Kimataifa hivyo hata muonekano wake na mazingira yake lazima yawe nadhifu.

Post a Comment

0 Comments